Wahamiaji 38 wakamatwa kwa kuingia Tanzania bila kibali

WAHAMIAJI 38 WAKAMATWA KWA KUINGIA NCHINI BILA KIBALI.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linawashikilia watu 38 wakiongozwa na Tadesa Limoli raia wa Ethiopia wote jinsia ya kiume kwa kosa la kuingia nchini kinyume cha sheria.

Taarifa iliyotolewa na kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya Kamishna msaidizi mwandamizi wa polisi Benjamini Kuzaga, inaeleza kwamba Watuhumiwa hao wamekamatwa Novemba 11, katika Pori la ranchi ya Matebete lililopo katika Kijiji cha Igumbilo Shamba, Kata ya Chimala, Wilaya ya Mbarali, wakisafiri kwa Gari yenye namba za usajili T.953 DJF aina ya Toyota Noah mali ya Stanslaus Mazengo.

Taarifa hiyo inaeleza kuwa Mtuhumiwa Stanslaus Mazengo ameeleza kwamba wahamiaji hao alikuwa akiwapeleka kuwahifadhi kwenye nyumba ya Jackline Malya Mkazi wa Chimala wakiwasafirisha kwa kificho kwa lengo la kuwapeleka nchini Afrika ya Kusini.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linatoa rai kwa baadhi ya wananchi wenye tamaa ya fedha kuacha tabia ya kuwawezesha raia wa kigeni kuingia ama kupita nchini bila kufuata utaratibu wa kisheria na badala yake wawaelekeze kufuata taratibu kupitia mamlaka husika ili kuepuka usumbufu ikiwemo kukamatwa na kuchukuliwa hatua za kisheria.