Kasi Ya Ujenzi Wa Uwanja Wa Mpira Wa Miguu Arusha Yaivutia Kamati Ya Bunge

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo imevutiwa na kasi ya utekelezaji wa ujenzi wa mradi wa ujenzi wa uwanja wa mpira wa Miguu Arusha ambao ujenzi huo upo mbele ya muda kwa kufikia asilimia 33 badala ya asilimia 31 iliyotarajiwa hadi sasa.

Kauli hiyo imetolewa leo Machi 13, 2025 jijini Arusha na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Husna Sekiboko wakati wa ziara ya kukagua ujenzi wa uwanja wa mpira wa miguu wa Arusha ambao unatarajiwa kutumika katika michuano ya AFCON 2027.

Aidha, Kamati hiyo imeitaka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kuendelea na kasi ileile ya utekelezaji wa mradi huo ili uwanja ukamilike kwa wakati na tija iliyokusudiwa.

“Kusema ukweli mradi unavutia na unafurahisha ni kwa sababu Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameamua kutoa fedha. Nina amini bila Rais kutoa fedha hata mkandarasi angekuwa mzuri namna gani asingeweza kufanya kazi. Kwa hiyo tunamshukuru na tunampongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri kubwa anayoifanya katika eneo hili la Habari, Utamaduni na Michezo hasa eneo hili la viwanja vya michezo” amesema Mhe. Husna Sekiboko

Kwa Upande wake Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Hamis Mwinjuma amesema ujenzi wa uwanja huo umefikia asilimia 33 na utakuwa na uwezo wa kuchukua watu 32,000 utakapokamilika June 2026, huku akieleza kuwa uwanja huo utakuwa uwezo wa kudumu miaka 130 ukiambatana na marekebisho ya kila baada ya miaka 10.