Jeshi la Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi linamshikilia mtuhumiwa Abdallah Ramadhan Mnolwa (24) Mdigo wa Iringa kwa kosa la kutoa taarifa za uongo.
Akizungumza na waandishi wa habari huko ofisini kwake Madema leo tarehe 14/04/2025, Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi ACP Abubakar Khamis Ally amesema mtuhumiwa huyo alifika kituo cha Polisi tarehe 10/04/2025 majira ya saa 3:00 asubuhi akidai amelawitiwa na watu anaowatambua kwa sura baada ya kutelekezwa na mwenyeji wake.
ACP Abubakar ameeleza kwamba baada ya kupokea taarifa hizo, Jeshi la Polisi lilifungua kesi na kuanza taratibu za kiupelelezi ambapo mtuhumiwa alipelekwa hospitali ya Mnazi Mmoja kwa ajili ya uchunguzi wa kitabibu, ambapo ilibainika kuwa hakuwahi kulawitiwa.
Amesema wakati Jeshi la Polisi linaendelea uchunguzi lilibaini kuwa taarifa zake ni za uongo na alishawahi kufanya matukio kama hayo wilaya ya Wete Mkoa wa Kaskazini Pemba mwezi Machi, 2025.
Aidha Kamanda ameeleza kwamba mtuhumiwa amekiri kufanya matukio hayo kwa lengo la kujipatia kipato kutokana na ugumu wa maisha.
Hivyo, Jeshi la Polisi linatoa onyo kwa yeyote mwenye kufanya vitendo vinavyoenda kinyume na sheria na kuleta taswira mbaya nchini hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake.
Leave a Reply