Padri Kitima aadhimisha misa ya shukrani baada ya kutoka hospitali


Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) Padri Dkt. Charles Kitima ameongoza Adhimisho la Misa Takatifu ya shukrani kwa mara ya kwanza baada ya kutoka hospitali alikokuwa anapatiwa matibabu kwa takribani mwezi mmoja baada ya tukio la shambulizi dhidi yake.


Padri Kitima ameongoza adhimisho hilo katika Kanisa la Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili lililopo TEC-Kurasini, Dar es salaam leo Juni 3, 2025 pamoja na mapadri, watawa na wafanyakazi wengine wa Sekretarieti ya TEC, kwa nia ya kumshukuru Mungu kwa kumponya.


Akitoa homilia katika adhimisho hilo Padri Kitima amemshukuru Mungu kwa kumponya dhidi ya shambulizi lililolenga kukatisha uhai wake, huku pia akiwashukuru watu wote kwa sala na matashi mema katika kipindi chote cha matibabu yake.


“Tunamshukuru Mungu kwa wema wake, pia tunawashukuru watu wote walioguswa na tukio lile. Tuombe ili Kanisa lizidi kuwa imara siku zote bila kutetereka. Tukumbuke kuwa Kanisa Katoliki ni taasisi inayotegemewa na watu wengi, ni sauti ya watu wasio na sauti, ni msindikizaji wa wanyonge. Tuliombee Kanisa letu lizidi kuwa mwanga na matumaini ya Watanzania” ameeleza Padri Kitima.


Aidha Padri Kitima amewataka wana Sekreatarieti ya TEC kuyapokea mambo yote yaliyotokea kwa jicho na moyo wa imani akisisitiza kuwa katika mambo yote ambayo Kanisa linayasimamia kwa ajili ya wanyonge, Mungu atayasikiliza.


“Mungu hatakaa kimya, atajibu sala zetu. Tuwe imara katika kazi zetu, tukumbuke kuwa hata mitume walipata misukosuko. Tusirudi nyuma, tubaki katika imani thabiti” ameongeza.