Argentina imeendelea kuthibitisha ubabe wake katika soka la Amerika Kusini baada ya kuichapa Brazil 4-1 katika mchezo wa kufuzu Kombe la Dunia, uliopigwa kwenye Uwanja wa Estadio Mas Monumental, Buenos Aires.
Matokeo ya Mechi
Argentina ilianza kwa kasi na kupata bao la mapema dakika ya 4 kupitia kwa Julian Alvarez. Kiungo chipukizi Enzo Fernandez aliongeza la pili dakika ya 13, kabla ya Alexis Mac Allister kufunga la tatu dakika ya 36. Brazil walijibu kupitia kwa Matheus Cunha dakika ya 27, lakini Giovanni Simeone alihitimisha ushindi mnono kwa Argentina kwa kufunga bao la nne dakika ya 71.

Argentina Yafuzu Kombe la Dunia
Kwa ushindi huu, Argentina imethibitisha rasmi kufuzu kwa Kombe la Dunia 2026, baada ya Bolivia kushindwa kuifunga Uruguay. Ushindi huu pia unaifanya Argentina kuendelea kuongoza msimamo wa kufuzu kwa Amerika Kusini (CONMEBOL), wakidhihirisha ubora wao kama mabingwa wa dunia.

Brazil Yazidi Kuwa na Rekodi Mbaya Dhidi ya Argentina
Kwa upande wa Brazil, matokeo haya yanaongeza changamoto kwao, kwani sasa wameshindwa kuifunga Argentina katika mechi tano za mwisho walizokutana. Timu hiyo inayoshikilia rekodi ya kuwa taifa lenye mafanikio zaidi katika soka la dunia, inaendelea kupitia kipindi kigumu katika safari yao ya kufuzu.

Mechi hii ilikuwa ikitarajiwa kuwa na kivutio kikubwa cha upinzani wa mastaa wawili, Lionel Messi na Neymar, lakini wote walikosekana kutokana na majeraha madogo.
Mwamuzi: Andres Jose Rojas (Colombia)
Uwanja: Estadio Mas Monumental, Buenos Aires, Argentina.
Argentina inazidi kuonyesha kuwa wao ndio mabingwa wa kweli wa soka la Amerika Kusini, huku Brazil wakilazimika kutafuta njia ya kurudi kwenye ubora wao wa zamani.
Leave a Reply